Monday, May 11, 2015

JAMBO 1 LA MSINGI KAMA UNATAKA KUFANYA KAZI KWA MAFANIKIO NA MZUNGU

photo by everystockphoto.com
Nianze kuelezea tatizo linalokwamisha watu wengi katika kufanya kazi na wazungu ukiachana na tatizo la lugha. Ipo namna hii, kwa kawaida katika mahusiano yetu ya elimu, kazi na biashara kibongo bongo ni kawaida sana kupeana ahadi zisizokamilika. Ninapozungumzia ahadi naamanisha hata kule kukubaliana kukutana saa fulani halafu mtu asitokee kwa muda mliokubaliana nako ni kuvunja ahadi. Ila kuna kasumba nyingine mbaya sana ya kuahidi kufanya shughuli fulani au kumpatia mtu kitu fulani siku fulani na wala usimpatie mtu husika au ukampatia ila kwa kuchelewa tena baada ya kukumbushwa naye mara kwa mara. Hali hii wenyewe tunaiita uswahili.

Uswahili huo upo katika biashara, katika elimu , na hata makazini. Nimeishi na kufanya kazi kwa muda mrefu na watu kutoka bara la Ulaya na Amerika ya Kaskazini hususani toka Marekani, Uingereza na Ujerumani na kushuhudia jambo linalowapa shida sana katika mahusiano yao na sisi waswahili ni huo uswahili kwakuwa pamoja na kuwa huko kwao wapo wanaotokea kutotimiza ahadi nyakati fulani, ila kwa ujumla watu wengi wakiwa katika mambo ya msingi katika elimu, biashara na kazi hutunza ahadi wanazotoa.

Wazungu wanajifunza toka wadogo kuwa ili ukubalike katika jamii inakupasa kumaanisha unachosema utafanya, kwa maana ya kwamba kutokutimiza ahadi ya jambo ambalo ni wewe mwenyewe ulisema ungefanya ni kujikanusha na kujionyesha mbabaishaji, usiyefaa kuaminika, na hivyo watu watakugwaya kwenye mahusiano nawe kwa mambo ya msingi.

Pia wanajifunza kutegemea wengine kutimiza wanayosema hivyo wao nao kupanga mambo yao kuendana na ahadi na mipango wanayofanya na wengine. Wazungu wengi wana mazoea ya kuwa na mipango ya muda mrefu, hata appointments (ahadi za kukutana na watu) huwa wanaziandika katika diary au sehemu nyingine kama kwenye simu ili waweze kukumbuka na pia kama itatokea kutaka kufanya appointment nyingine kwanza hucheki orodha ya appointments ambazo tayari wamekwishaweka.

Kujifunza kwao kuheshimu ahadi kunaendana sambamba na kuwahi au kufika kwa muda ule ule mliokubaliana mkutane kwakuwa kutokufika kwa muda mliokubaliana ni kuvunja ahadi, na kuvunja ahadi ni dalili ya kutokuthamini na kumheshimu mtu mwingine na muda wake.

Kinyume chao, sie bongo, wengi tumezoea kuwa ahadi ni maneno tuu na kuwa inawezekana tuu kutoa kisingizio cha kutotimiza ahadi husika bila tatizo. Ndio maana mtu hata kama anajua hatoweza kufanya jambo kwa muda fulani , yeye huamua kusema atafanya, ila itatokea kutokulifanya na huja na visingizio vya “maana” kujitetea kwa nini hakutimiza alilosema angefanya.

Sie kibongo bongo pia wakati wa kukutana(appointment) tayari katika akili zetu tunakuwa tumeshategemea kuwa mwingine atachelewa, na wala haitusumbui akilini kuwa kutokufika kwa muda uliopangwa ni tatizo kwani daima mtu huja na sababu “nzito”.

Nimeshuhudia “waswahili” kadhaa wakikosa fursa za kufanya mambo ya maana na wazungu kwakuwa wazungu husika hawakuwa na muda wa kuvumilia kama wabongo tunavyovumilia huo uswahili. Wapo wabongo ambao hutimiza makubaliano yao “kizungu” na hivyo wazungu wanaowapata watu wa namna hii hudumu nao sana.

Hivyo kama unataka kazi au mahusiano yenye tija na endelevu na wenzetu wengi wa nchi za magharibi, jifunze kuwa mtu wa maneno yako. Usiahidi usichoweza kutimiza, hakikisha kabla ya kukubali au kuahidi kufanya jambo fulani unachunguza mipango yako ya muda mrefu, unachunguza changamoto zako na vikwazo ambavyo pengine vitakukwamisha kutotimiza ahadi. Weka ahadi unazoweza kuzitimiza. Na kama inatokea jambo ambalo hukulitambua mapema kama kikwazo mtaarifu mtu husika uliyemuahidi mapema na sio kukaa kimya mpaka wakati wa ahadi au mpaka mhusika akuulize.


Hata wewe unaweza kuwa “mzungu”. Hii inawezekana kwa kuanza kuamini kuwa unaweza kubadilika na kuwa hali  ya “uswahili” si njia sahihi ya kuishi kiungwana na si njia ya kuonyesha unawajali wengine. Thamini muda wa wengine, thamini mipango ya wengine inayotegemea kutimiza ahadi zako, wapende na kuwajali wengine , nawe upendo na kujali huko kutakurudia na utapata manufaa kibao katika maisha yako.

Tuesday, May 5, 2015

WAFAHAMU WATU HATARI WANAOJULIKANA KAMA SOCIOPATH

Dexter Morgan katika tamthilia iitwayo DEXTER anaonyesha tabia
zinazotambulisha Sociopaths. Itazame hiyo tamthilia kwa kujiongezea
ujuzi kuhusu watu hawa hatari waitwao sociopaths.
Hii ni kwa mujibu wa mtaalamu aitwaye Paul Rosenberg na references nyingine. Atakayetaka makala nzima aniambie email yake ntamtumia.

Kwanza sociopath ni nani ? A sociopath: is an otherwise normal human who has a profound lack of empathy for the feelings of others.  Yaani sociopath kwa asili yeye haoni huruma kwa mtu yoyote yule. Hata hivyo sio lazima ajionyeshe wazi wazi kuwa hana huruma, hujificha ili kutimiza hitaji lao la kumpata mtu wa kumtenda.
Kwakuwa wao hawana hisia zozote za huruma wala mapenzi, inawalazimu hao sociopath kuiga watu wa kawaida wanavyoishi. Na kwakuwa hatutilii maanani jinsi watu wanavyoonekana , ni ngumu kutambua nani haswa ni sociopath, nani siye.
Ni shida kumjua sociopath kwakuwa
1. Wengi wetu tunaamini kila mtu ni mzuri, wakati ukweli kuna watu 100% ni wabaya tuu, ni muda tuu unawasubirisha kufanya ubaya wao.
2. Sio wengi sana inakadiriwa 2% ya watu wote ni sociopath mahesabu ambayo pia yanasemwa kuwa kati ya watu 50 mmoja ni sociopath
3. Lingine kwakuwa wao hawana hisia yoyote wao hawajisikii vibaya kudanganya, jambo linawapelekea kutokutambulika uongo wao hata kwenye LIE DETECTERS, zile mashine za kutambua kama mtu anasema uongo au la.
Baada ya kueleza hapo juu kwanini ni ngumu kwa watu wengi kumtambua sociopath tuone jinsi ya kumtambua.
1. Kama unasoma hii kitu tayari unafaida ya kumtambua sociopath kwakuwa wao hutumia kutokujua kwetu kuwa wao wapo. Ile imani kuwa kila mtu mzuri hutuharibu na kutuweka hatarini kudhurika na sociopath. Hivyo kila wakati tambua kusoma jinsi mtu anavyobehave.
2. Pamoja na kwamba sociopath huiga kuonekana wapo wa kawaida, huwa wanashindwa kwa asilimia 100 kuonyesha huruma na upendo. Ingawa wengine huwa na wenza wa ndoa, na hata watoto, ila chunguza namna wanavyoonyesha hisia zao haswa utagundua utofauti mkubwa. Vitu vya kuangalia ni namna wanavyojali wapenzi wao, watoto, mambo ya misiba na mijumuiko ya kijamii,  pamoja na kuweza kufeki, ila ukia ngalia kwa makini utajua kuna walakini.
3. Kwakuwa sociopath kiasili hujisikia raha kudhuru wengine , chunguza watu ulionao karibu  je hujisikia raha kusingizia wengine, au hufanya matendo  yasiyo ya kihuruma na hawaonyeshi kujutia, n.k .
4. Wazungu wanasema "when the deal is so good, think twice". Kuwa makini na watu wanaojifanya wema sana.
5.Kwakuwa wanahitajika kujificha, hujitengenezea mazingira ya kutokutambulika na kuiaminisha jamii kuwa ni watu safi, kiasi kwamba hata ukija sikia wamefanya hivyo utashangaa. Wengi wa wanasiasa  na viongozi wa asasi mbalimbali inasemekana ni sociopath.
Chunguza maamuzi ya wanasiasa wengi yasivyo na huruma. Mfano wa viongozi maarufu ni Mao Tse-tung ambaye ni baba wa taifa la  CHINA anayedaiwa kubaka na kuua watu wengi kwa njaa. Mwingine ni kiongozi wa zamani wa shirika la utangazaji la BBC anaitwa Jimmy Savile ,yeye alikuwa na genge la udharirishaji wa watoto. Aliendesha genge lake kwa miaka 40 bila watu kujua, mpaka alipofariki.

Baadhi ya maswali ambayo watu wengi huuliza:

Je unajitambua kama  wewe ni Sociopath ?
Waweza jipima kama wewe ni sociopath au la. Je, unapata ugumu kuwaonea wengine huruma ? Je unapenda kuona wengine wanateseka au haujisikii lolote mtu mwingine anapoteseka ? Je, kwa makusudi umewahi kutaka kumfanyia "kitu mbaya" mtu ?

Je, sociopath kuna kitu kinatokea unakuwa triggered?
Sio lazima kitu kitokee wawe triggered, kumbuka hawa sociopath hawana hisia zozote

Je sociopath ni wazungu tuu kwa kuwa wazungu labda wanakuwa lonely so hawana cha kufanya kiasi kwamba wananyemelewa na hizo hisia?
Sociopath hajisikii lonely. Hajui hizo hisia za kuwa lonely , hajisikii kutaka kupendwa, hajisikii chochote. Huyo ndio real sociopath. Hata hivyo SIO kila mtu mwenye kufanya jambo la ukatili ni sociopath. Kuna wanaofanya jambo baya wakajutia, pengine kwa hasira , au visasi. Ila sociopath yeye , kufanya ubaya ni "hitaji" lake muhimu.

Serial Killers wote ni sociopath. Serial killers ni wale wanaojitengenezea orodha ya. watu wanaowaua. Ni hatari sana hawa watu, kwani sio lazima watumwe kuua. Ni kwamba wanajitengenezea sababu zao kichwani mwao zinazowatosha basi.
Hata hivyo SIO kwamba sociopaths wote ni serial killers.

Friday, May 1, 2015

DALILI 5 ZA MWENZA BORA WA NDOA

Ni kweli kuwa karibu vitabu vyote vya dini vinasisitiza kuwa na mwenza wa maisha kama njia sahihi ya kuishi maisha yako ya kimapenzi na pia kutimiza majukumu mengine ya kuendelezana kati ya jinsia hizo mbili. Katika makala hii mambo ya msingi ya kuepuka ili upate mke atakayekidhi maelekezo ya vitabu vya dini, yaani mke bora. Kabla ya kuenda mbali tujikumbushe vitabu vinasema nini kuhusu mke bora:
"Na katika Ishara zake ni kuwa amekuumbieni wake zenu kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao. Naye amejaalia mapenzi na huruma baina yenu. Hakika katika haya bila ya shaka zipo Ishara kwa watu wanao fikiri."--Qur'an 30:21 http://www.theholyquran.org/
Apataye mke apata kitu chema; Naye ajipatia kibali kwa Bwana. 
-         Mithali 18:22 https://www.wordproject.org
Sintokuchosha na mistari mingi toka vitabu vya dini, hiyo miwili hapo juu inatosha kueleza ubora na umuhimu wa kupata mwenza sahihi wa ndoa. Hata hivyo swali gumu linalowakwamisha wengi ni kuwa je unamjua mwanamke atakayeweza kuwa mke mwema ?

Usitegemee kumrekebisha wakati mmeshaoana: 
Ndoa sio uwanja au shule ya mafunzo kwa mke wako kuishi unavyotaka hivyo usitegemee kuoa mke mwenye tabia fulani usizozipenda kwa kujipa moyo akiwa katika ndoa atajirekebisha. Je asipojirekebisha ? Hapo ndo mwanzo wa migogoro isiyoisha.Unamkubali mke maana yake umemchunguza na kusema “namkubali” , na kama kuna madhaifu basi maana yake umekubali kuishi nayo kwani hata wewe pia una madhaifu yako.

Anaonyesha vitendo sio tuu maneno: 
Ni zaidi ya kuwa mcha Mungu kwa maana ya muonekano wa kuenda msikitini au kanisani, bali anaonyesha vitendo kuwa ni mwenye huruma, mpole kiasi, na mwenye kuthamini wengine.

Sio mfuata upepo:  
Mke bora ana uhuru wa fikra sio tuu dhidi ya wewe kukubaliana na kila jambo unalotaka , ila pia anakuwa na uwezo wa kuchambua anayoyasikia toka nje ya ndoa yenu na kubaki na mtazamo chanya wa mahusiano yenu. Hata kwa wewe mwenyewe hatokuwa mfuata upepo wa kila utakacho kwani kumbuka kuwa yeyé ni msaidizi wako, hivyo kuwa tayari pale atakapokurekebisha na kukukosoa .

Mdadisi na mwenye kujifunza
Nyote mnapoanza mahusiano mnakuwa na ndoto ya maisha ya furaha na mafanikio. Hata hivyo kadri siku zinavyoenda na mabadiliko ya kijamii, kiuchumi, na nyie wenyewe pia mnabadilika kitafakari  na kimahitaji. Mke bora atapenda kuwa mdadisi na kujifunza kukabiliana na mabadiliko haya ili kuendelea kutunza ndoa yake.


Mmejadili naye mambo ya msingi kuhusu maisha yenu ya baadae na unafahamu msimamo wake
Katika makala yetu ya  siku za nyuma tulijadili  kuwa kuna mambo 6 yanayoweza kuhatarisha mahusiano yenu kama hamtojadili na kufikia muafaka. Mambo hayo ni fedha, imani, mahala pa kuishi, watoto, falsafa ya maisha na  hisia za mapenzi. Soma zaidi BOFYA HAPA

Sunday, April 19, 2015

USIACHE KAZI ULIYONAYO: DALILI 7 KUWA HAUNA UWEZO WA KUJIAJIRI


1.Hauna Wateja Makini: Unashidwa kueleza kwa ufasaha wateja unaolenga hasa ni akina nani-yaani ni kundi gani la watu, na kwanini watu hao watanunua bidhaa yako. Haitoshi tuu kusema kwa mfano, utaanzisha kampuni ya mambo ya IT, au Advertising, lakini hauna maelezo ya kina akina nani hasa watanunua bidhaa unazotaka kuuza. Haitoshi kusema kwa mfano, “wateja wangu ni watu wote na asasi zinazohitaji huduma za IT, au Advertising,  inabidi uwe na uchambuzi wa kina aina gani ya watu na asasi zinazoweza kweli kuhitaji bidhaa zako, na kwanini unadhani watakuja kununua bidhaa zako. Kumbuka sio lazima uwe na majina ya asasi au watu unaotazamia waje wanunue kwako, ila kuwa na mtazamo wa kina wa tabia na wasifu wa kipekee wa wateja wako watarajiwa ni jambo la msingi.

2.Hauna Bidhaa Ya Kipekee:  Ili kuhakikisha unapata kipato cha kuridhisha na kuwa na biashara endelevu, inakupasa uwe na bidhaa ya kipekee katika kujiajiri kwako. Kama hauwezi kueleza kwa kifupi walau kwa sentensi tano, upekee wa bidhaa na uendeshaji wa biashara yako, ni dalili kuwa kujiajiri kwako hakutokuwa na tija.

3.Una haraka ya mafanikio:Mtazamo wako mkuu ni kujenga biashara yenye kukua ‘chap chap’, na pengine kwakuwa una mtazamo huu, una amini kuwa namna pekee ya wewe kuanzisha biashara yako ni kuwa kwanza na mtaji mkubwa wa kifedha. Ingawaje ni kweli kuwa fedha nyingi ni muhimu katika kuanzisha na kuendeleza biashara, mtaji mkubwa si wa lazima kwa kila aina ya biashara, na kwanza njia bora ya kuanzisha biashara ni kuanza kidogo kidogo. Hata biashara kubwa kama kampuni ya Apple inayotengeneza simu za iPhone – ilianzia tuu kwenye kachumba kadogo ka gereji, kampuni ya kompyuta ya DELL-inayotengeneza kompyuta aina ya Dell, ilianza kwenye kachumba kadogo ka bweni la chuo, tena kwa mtaji wa $1000 tuu !.

4.Hauna Mtandao wenye tija:Ni wazi kuwa watu watakaotoa mchango mkubwa katika mafanikio ya biashara yako ni wale ambao unamfahamiana nao kwa karibu, kupitia mtandao wako. Haitoshi tuu kufahamiana na watu wengi, bali watu hao wengi wakufahamu pia haswa haswa wakufahamu kwa mazuri na uwezo wako katika mambo makubwa, ni rahisi hapo baadae kupata humo katika mtandao wako, washirika wa biashara, wateja na hata wasambaji wa bidhaa na huduma kwa biashara yako. Na kama inavyosemwa: “ Katika dunia tuliyopo sasa, sio tuu una nini na una jua nini, bali je unamfahamiana na akina nani ?”

5.Hauna mkakati maridhawa wa kifedha:Biashara utakayoianza itahitaji fedha na pia wewe binafsi na familia yako mtahitaji fedha. Kwa kuwa ni muhimu kuweka tofauti mambo ya biashara na mambo yako binafsi, ni unatakiwa uwe na mkakati wa maridhawa wa kifedha wa matumizi na mapato yako binafsi na  yale ya biashara.Hata kama unafikiria kuwa biashara itakuingizia fedha za kujikimu na kusukuma maisha, je mapato kuchukua kwako huko fedha toka kwa biashara kutaathiri vipi mwenendo wa biashara, ambayo ndiyo itakuwa chanzo kikuu cha ajira yako?

6.Hauna Ufahamu wa kutosha kuhusu biashara uitakayo:Ufahamu wa biashara utakayo kuianzisha ni muhimu kwani utakuwezesha kujua kama kweli inalipa au la, na pia kujua mbinu za kuiboresha na kuifanya endelevu kwa siku za usoni. Ufahamu wa kutosha wa biashara utakuwezesha kutafakari pia kwa undani wateja gani hasa unawalenga, washindani gani hasa utakabiliana nao, na pia changamoto na matatizo ya biashara husika kabla haujaingia kuianza.

7.Hauna mvuto wa kutosha kwa biashara uitakayo kuanzisha: Unahitaji kusikia kitu kama wito au mvuto wa kipekee wa kitu unachotaka kukifanya kama biashara ili kweli uweze kukifanya kwa uendelevu , kwani kutakuja nyakati ambapo biashara haitaingiza kipato cha kutosha, utapitia changamoto na matatizo mengi, na wakati huo, kitu kitakachokupa msukumo wa kipekee wa kuendelea na kuwaongoza hata washirika na wafanyakazi wako muendelee na biashara, ni kule kupenda (wito) wako na hiko unachotaka kukifanya kama biashara.

"SUMU" 6 ZA UCHUMBA: MAMBO YA KUZINGATIA KABLA YA NDOA

Ukweli ni kuwa watu wawili wanapoamua kwa dhati kuwa katika mahusiano ni kwamba wanakuwa tayari katika akili zao wamejenga matarajio au matumaini ya kunufaika na uhusiano husika, hata kama hawawezi ambiana moja kwa moja kuwa “ aisee, mie kuwa na wewe nataraji moja , mbili, tatu….”.
Kunapokuwepo na upendo, basi pia kunaleta majukumu, ambapo bila ya kutimizwa kwa majukumu yanayotarajiwa kutimizwa, maana halisi ya mahusiano bora inapotea.
Hii si tuu kwa mahusiano ya kimapenzi, bali hata dini zinatufundisha kuwa Mungu anatupenda, na katika hilo, tunajukumu la kutii amri zake, na kwamba tusipotii amri zake, tunakuwa tumeharibu maana nzima ya upendo wake, kwani tutajikuta tumeingia motoni/jehanamu (Kinyume cha upendo).
Hata katika familia, tumesikia mzazi pamoja na upendo alioonyesha kwa mtoto wake toka yupo tumboni mpaka mtoto ameweza kujitegemea, endapo mtoto husika akashindwa kumjali ( hili ndio jukumu linalokuja na upendo wa mzazi), basi unaweza sikia mzazi huyo akitoa ‘laana’ au ‘akamwachia radhi’ mtoto wake mwenyewe wa kumzaa.
Ni wazi kuwa mara nyingi majukumu yanayoletwa na upendo huwa hayaelezwi wazi wazi, hata hivyo katika mahusiano, mambo yafuatayo yanaweza kuwa sehemu ya matarajio ambayo  wapenzi wanaweza kuwa makini ili waweze kuwapendeza wenzao. Kwa maana nyingine ni kuwa yafuatayo, ndio maeneo ambayo mtu aliye kwenye mahusiano ni muhimu ‘acheze’ vema ili kulinda mahusiano/penzi:-

Fedha:  Katika swala la fedha, jambo kubwa linalojitokeza ni namna ya kufanya maamuzi kuhusu matumizi ya fedha.  Ni muhimu kuweka mikakati ya pamoja kwa mambo ya msingi kimaisha , na kila mmoja kutilia maanani mipango hiyo, kabla ya kuamua kutumia kipato chake kwa mambo ambayo pengine hayapo nje ya mipango ya kifedha ya wawili nyie kama wapenzi.  Bila shaka, kuendana na aina yenu ya kipato, aina yenu ya maisha, kama wapenzi mtakuwa na kiwango fulani cha fedha ambacho si busara mmoja wenu kuamua kutumia bila kumtaarifu mwenzake , hata kama matumizi husika ni muhimu sana, na haijalishi nani kazitafuta fedha husika.

Imani: Katika swala la imani, ni muhimu kufahamiana vema mwenendo wa kiimani wa mwenza wako, na kuheshimu kuwa swala hili ni nyeti, na mabadiliko ya kweli hayawezi kulazimishwa. Imani inaweza athiri namna mnavyoweza kuwasiliana kama wapenzi – kwani mwingine mwenye msimamo mkali wa kidini, anaweza kukataa jambo fulani hapo baadae, jambo ambalo pengine mwenza wake anaona ni jambo la kawaida tuu. Imani inaathiri malezi ya watoto, na inaweza athiri shughuli za kiuchumi za wawili nyie, mfano pale mmoja wenu anapoamua kujikita katika  ‘huduma’ zaidi, kuliko familia na shughuli za kuingiza kipato.

Mahali pa kuishi:  Mtaa gani , wilaya gani, mkoani gani, nchi gani au bara gani kila mmoja wenu anatazamia muishi ni jambo la msingi kuliweka wazi kati yenu. Jambo hili linaweza kuendana na mambo mengine mengi ambayo yanachochea mabadiliko ya muda mfupi na hata muda mrefu katika maisha yenu, kama vile , aina ya kazi mnazotarajia kila mmoja wenu kufanya, na aina ya kazi unazotamani au kufikiri ni vema mwenza wako afanye.

Watoto: Hili ni jambo zito haswa katika vipengele vya lini watoto wapatikane (ujauzito), idadi ya watoto, aina ya malezi kwa watoto watakaopatikana, na zaidi sana majukumu ya kifedha katika malezi ya watoto (mfano, nani atalipa ada ya shule, n.k). Pamoja na kutafakari hayo, watu wawili mlio katika mahusiano, ni muhimu mkatengeneza picha ya maisha ya watoto wenu endapo mmoja wenu atatangulia mbele za haki (atafariki), na hata ikiwezekana  mwaweza fikiria na kupanga aina ya maisha mnayotaka watoto wenu waishi pale nyote wawili hamtokuwepo  duniani. Inapotokea mambo kama hayo yaliyotajwa hapo juu hayajawekwa wazi mbele yenu, ni rahisi mmoja wenu kufanya mambo yasiyompendeza mwengine –mfano wakati mwingine anafikiria akiba ya baadae ya watoto ili wakasome international school, mwingine anafikiria namna ya kutanua ili ‘kuuza sura’.

Falsafa ya maisha:  Swala hili linahusu wa kipekee na tafakari huru ya kila mmoja wenu kuhusu mambo kadhaa ya kimaisha kama vile mtazamo wa kila mmoja wenu kuhusu biashara (mwingine biashara ni kitu cha kuweka heshima kwa jamii, wakati mwingine biashara ni kielelezo cha huduma kwa jamii na hivyo kinahitaji muendelezo).
Falsafa pia inahusu namna kila mmoja wenu anavyochukulia mambo kama vile kusaidia watu wengine, kuwa na mahusiano na watu wa jinsia tofauti (wapo wasiotaka hata classmet ampigie simu mpenzi wake). Falsafa pia inahusika na namna kila mmoja anavyotafsiri mafanikio katika maisha, na alivyo tayari kufanya yanayopaswa kufanywa kufikia mafanikio (Mfano, wengine mafanikio ni mali na umaarufu, wakati kwa wengine mafanikio ni namna anavyoweza kuwa na furaha na uhuru , pamoja na kusaidia wengine).
Katika juhudi za kufikia mafanikio unawea kukuta wapenzi mnatofautiana kwani mmoja anaweza amini rushwa ndio suluhisho pekee la kufikia anakotaka, wakati mwingine anaamini tofauti na hivyo.  

Hisia za kimapenzi: Ni jambo la msingi kutokupuuzia hisia za kimapenzi za kila mmoja wenu. Tambua vile mwenzako angependa akuone unamvutia na vile ambavyo unamjali hisia zake. Ni kweli kuwa katika mahusiano, hisia za kimapenzi zinaweza zisichukue nafasi kubwa kati yenu kwani kuna mambo mengi ya kufanya pamoja kama wapenzi, hata hivyo pamoja na udogo wake wa muda, jambo hili nyeti lisipopewa kipaumbele, linaweza sababisha mengine yote kuharibika. Zaidi sana, kumbuka wewe na mpenzi wako, ni watu wa jinsia mbili tofauti, kinachowafanya muungane kiasili ni hizo hisia za mapenzi kati yenu.

Hitimisho: Sio lazima kama watu wawili mlio katika mahusiano muwe na mtazamo sawa katika hayo yote yaliyoelezwa hapo juu, hata hivyo, ni muhimu sana kwenu nyote kuwa na picha kichwani ya mtazamo wa mwenza wako kuhusu mambo hayo niliyotaja hapo juu.
Pale mnapokubaliana kutofautiana katika mambo yaliyotajwa hapo juu (mf.mambo ya fedha, na imani), hakikisheni mnakubaliana bila kutofautiana kuhusu athari za kutofautiana kwenu, na jukumu la kukubali athari hizo kwa mahusiano yenu.

JIPIME HIVI KAMA UNATAKA DILI KALI

Angalia jinsi maisha yanavyozidi kuwa magumu katika jamii zetu. Gharama za vyakula, usafiri, na mambo mengine zinazidi kuongezeka, pia mabadiliko ya kiteknolojia na kijamii yanaleta changamoto nyingi. Tupo katika zama ambapo kusimama kiuchumi kunahitaji kujidhatiti kweli kweli. Makala hii inachambua mambo ya msingi ambayo yanaweza kukusaidia kujipanga kupata dili zinazoweza kuinua maisha yako.

1. Jitafakari: 
Ni vizuri kujizoesha kutafakari kuhusu wewe ni nani, mapungufu yako, mambo gani makubwa na mazuri uliyokwisha wahi kufanya, na vitu gani hasa unavipenda na usivyovipenda. Tafakari hii itakupa picha ya aina gani ya mtu wewe ulivyo, na kukusaidia kujipanga kuziba yale mapungufu, na wakati huo huo, utaweza kuangaza fursa zilizopo na unazoweza kuzitumia kutokana na 'ubora' ulionao.
Tafakari hii itakuwezesha pia kutambua kitu kiitwacho kwa kiingereza 'passion', yani mambo unayoyapendelea sana kufanya au kuwa hapo baadae. Umuhimu wa kutambua passion ni kwamba ukiweza kuwekeza muda katika passion yako inaweza kuwa sehemu nzuri ya kujijengea maisha yenye furaha. Kwani passion itakufanya ufanye jambo utalotaka kulifanya kwa ufanisi na pia hata ukikumbana na changamoto, hautokata tamaa kirahisi rahisi.

2. Mambo mazuri hayataki haraka
Kumbuka hao wote unaowaona wamefanikiwa kimaisha, mafanikio ambayo pengine unatamani uwe nayo, sio kwamba mafanikio hayo yalikuja kwa siku moja. Kuna maandalizi kadhaa waliyafanya, magumu waliyoyapitia mpaka kufika hapo walipofika.
Hii kwako ina maana kuwa ni lazima ujue kuna muda ni lazima uutumie kufanya maandalizi, inabidi utambue kuwa utakutana na magumu, ila hautakiwi kukata tamaa. Na zaidi sana ni lazima ujue bidii inahitajika. Hata hivyo bidii zako zitazaa matunda kwa haraka kama utatambua mapungufu yako mapema, na pia passion yako hasa ni ipi. Ukitambua mapungufu yako mfano una tatizo la lugha ya kiingereza, basi utafanyia kazi pungufu hilo ili uwe bora zaidi.

3.Utafiti ni muhimu sana
 Ni muhimu sana kuwa na taarifa sahihi kuhusu nini vinaweza kufanikisha  mipango yako na matarajio yako ya kimaisha. Mfano kama unatamani kufanya biashara, basi tafakari aina gani ya biashara, tafuta taarifa za kutosha kuhusu wateja wa biashara husika, kiasi cha mtaji , mbinu za kimasoko , n.k Vyote hivyo vitakuwezesha kujipanga kwa ufasaha ili kupunguza hasara na muda mrefu wa kufikia mafanikio.
Hii pia inahusika katika aina ya kazi unayotamani kufanya, je ni kwa kiwango gani utahitaji lugha ya kigeni, uwezo wa kutumia teknolojia mpya, kiwango cha elimu , n.k

4.Kubali kuwa tofauti
Wewe na yule mna historia tofauti za maisha, malezi tofauti, tabia tofauti, na hata uwezo wa kufikiri na hisia tofauti. Vyote hivi vinaweza kuchangia katika namna tofauti za kukabiliana na changamoto za kimaisha, na hata katika kupata fursa. Hivyo basi badala ya kuwaza kutaka kuwa kama fulani, tafakari nini wewe kama wewe unaweza kufanya, kiwango gani cha uvumilivu na juhudi kinahitajika ili kufikia malengo yako, na jitahidi kufanya unayotakiwa kufanya kwa juhudi.
Hakuna  'shortcuts' za mafanikio. Na mafanikio ya 'kulazimisha' hayawezi kukuletea furaha ya kweli maishani mwako.
Utakuja kugundua kuwa la msingi sana katika maisha ni kuwa na furaha na amani ya moyoni.

HITIMISHO
Kujitambua mapungufu yako na kuyarekebisha , halafu ukatambua pia mambo uliyo mzuri sana katika hayo, kisha ukazitumia fursa zinazoendana na hayo, kutakufanya ujiweke katika namna nzuri ya kupata dili za kuboresha maisha yako.
Hata hivyo kwakuwa mafanikio ni safari , unapaswa kujipanga kwa kuwa na taarifa sahihi, kuwa na bidii endelevu katika mambo ya msingi, na zaidi sana uweze kujitofautisha na wengine ili uweze kutambulika ubora wako, na hatimaye dili kali zije kwa ajili yako.

MICHONGO YA AJIRA NJE YA TANZANIA IPO HIVI..

Aina za kazi

1. Kazi zenye mahitaji maalum : 
Hizi ni kazi za fani mbalimbali ambazo serikali za nchi kadhaa hutangaza kuwa nchi husika inahitaji sana watu wa fani husika. Serikali ya nchi husika hutoa muongozo wa jinsi mashirika/asasi mbalimbali zinavyoweza wasilisha maombi ya mahitaji maalum ya kuajiri.Mfano nchi kama Afrika Kusini mwaka 2011 ilitoa muongozo ufuatao. Bofya hapa kusoma.
La msingi kukumbuka hapa ni kuwa uhitaji maalum huu sio kwamba serikali ndio inahitaji kuajiri watu hapana, ni taifa kwa ujumla- serikali, mashirika na makampuni mbalimbali ya nchi husika yanahitaji kuajiri watu wa hizo fani zenye mahitaji maalum.  Kwa msingi huu,michakato na taratibu za uhamiaji –kutoa vibali vya kazi, huwa si ngumu sana kama ilivyo katika aina nyingine za kazi.

2. Kazi zenye ushindani: 
Hizi ni kazi ambazo si lazima ziwe zimetangazwa kuwa za mahitaji maalum kwa taifa, hata hivyo mashirika na makampuni ya nchi husika hushindana katika kupata watu bora wa kufanya kazi husika. Mfano wa kazi hizo ni graphics designers,

3. Kazi za kawaida: Hizi ni aina  nyingine ya kazi ambazo haziingii katika makundi yaliyotajwa hapo juu. Mfano kazi za mikataba ya muda mfupi, kubadilishana wafanyakazi –mfano mtanzania kuhamia Kenya na Mkenya kuhamishiwa Tanzania. Kundi hili pia linajumuisha ajira kwa wanamichezo na wasanii.

Jinsi ya kupata taarifa za ajira za nje ya Tanzania
 Unaweza kupata taarifa za nafasi za kazi zilizopo huko nje ya Tanzania kwa kupitia njia mbalimbali kama vile:-
1.Marafiki/Ndugu na jamaa waishio nje ya Tanzania:  
Kwa kutumia marafiki , ndugu , na jamaa ambao wana taarifa sahihi na zinazoweza kukusaidia kuhusu soko la ajira, unaweza kujikuta unapata taarifa muhimu. Nafasi nyingi zinaweza kuwa zinapatikana ila hazitangazwi kwenye vyombo vya habari , hivyo marafiki, ndugu , na jamaa waishio huko nje ya Tanzania, wanaweza kukudokeza ‘michongo’ iliyopo na jinsi unavyoweza kuifanyia kazi. Ni muhimu kudadisi vema ili ujue aina ya kazi, sifa zinazohitajika , malipo na mazingira ya kazi kabla haujafanya maamuzi ya kusafiri kwenda kuapply au kufanya interview.

2.. Mitandao ya kijamii:
Ukitembelea baadhi ya pages za mashirika na makampuni hutangaza nafasi za kazi kwa kurasa zao za mitandao ya kijamii. Mfano mzuri ni  Microsoft Africa kama unavyoweza jionea tangazo hili hapa chini kwenye picha, toka kurasa yao ya Facebook:
3. Website za Makampuni na Mashirika:   
Tembelea websites na hata blogs za mashirika na makampuni mbalimbali yaliyopo nje ya Tanzania, na tazama kama wameweka tangazo/matangazo ya nafasi za kazi.

4. Website za mawakala wa ajira (Recruitment Agents):   
Kuna mashirika au makampuni maalum yanayojishughulika na kuajiri kimataifa. Mawakala hawa hutangaza nafasi za ajira na pia hutoa maelezo ya mchakato wanaotumia kufanikisha mtu kupata ajira. Hata hivyo kuwa makini na mawakala hewa wanaotanguliza kudai malipo. Baadhi ya Mawakala wa ajira na websites zao ni kama ifuatavyo:

5.Websites za watangazaji wa ajira:
Kuna websites kadhaa zenye kujishughulisha na kuweka hewani matangazo ya ajira kutoka mashirika, makampuni mbalimbali na mawakala wa ajira. Unaweza ku search kwa kutumia Google kwa kuandika neno mfano Accounting jobs in Sudan, na kupata maelezo majibu ya Google yakiorodhesha  websites za watangazaji wa ajira au websites za mashirika/makampuni husika. Pia waweza tembelea websites za watangazaji wa ajira maarufu kama vile:

6. Linkedin: 
Mtandao maalum kwa watu wa fani mbalimbali, ambapo pia makampuni na mashirika mbalimbali hutangaza nafasi za ajira. Pia waweza chagua huduma ya Linkedin ambapo utakuwa ukitumiwa taarifa za nafasi za kazi kwa kadri ya uzoefu na ujuzi wako uliorodhesha katika wasifu wako, na pengine kwa uchaguzi wa aina ya nafasi za ajira unazotaka kufahamu. Usisubiri mpaka utumiwe matangazo, waweza tembelea kurasa husika za mashirika na makampuni humo Linkedin na kutambua nafasi za ajira zinazotangazwa.

Taarifa kutoka kampuni au shirika ulilopo sasa: Pengine kampuni au shirika ulilopo lina utaratibu wa kubadilisha  maeneo ya kazi ya wafanyakazi wake. Fuatilia kujua mchakato mzima wa kubadilishwa eneo la kazi upoje, masharti na lini mabadiliko (transfer) hayo hufanyika. Hii inaweza kuwa nafasi yako ya kujiandaa kuhamishiwa nje ya Tanzania kwani waweza kutambua vigezo ya kiutendaji au kielimu unavyotakiwa kuwa navyo ili upewe ‘promotion’ ya kuenda nje ya Tanzania.

Masharti ya kufanyakazi nje ya Tanzania

1. Uhakiki wa vyeti vyako:  
 Baadhi ya nchi za nje hutaka kuwa waombaji wote wa vibali vya kazi wahakiki vyeti vyao kupitia mamlaka au taasisi maalum ya nchi hizo ili kujiridhisha kuwa kweli vyeti vyako ni halali, na kwamba aina ya kiwango cha elimu ulichonacho kinaendana na viwango vya elimu vya nchi hizo.

2. Kuandikishwa katika mamlaka au wakala fulani wa fani husika:  
Baadhi ya nchi za nje hutaka kuwa waombaji wote wa vibali vya kazi wawe wamehakikiwa na kuandikishwa na mamlaka zinazohusika na fani ambayo muombaji wa kibali cha kazi anataka . Mfano kama ni mhasibu basi awe ameandikishwa na bodi ya wahasibu ya nchi husika.

3. Kuwa na Passport: 
Ni lazima uwe na passport halali na pia isiwe imeisha muda wake, na kwamba wakati wa kuomba kibali cha kazi , ni lazima uwe na viza isiyoisha,yaani bado una uhalali wa kuishi nchi husika walau kwa mwezi mmoja zaidi kama unafanya maombi ya kibali cha kazi ukiwa katika nchi husika huko ughaibuni.

4. Malipo ya kibali cha kazi: 
Malipo ya kibali cha kazi, hutofautiana kati ya nchi na nchi.

5.Taarifa ya polisi: 
Hii ni taarifa ambayo polisi nchini Tanzania wataitoa kueleza kuwa wewe si mhalifu au mhalifu. Kabla ya polisi kutoa taarifa hii hufanya uchunguzi wa maabara wa alama zako za vidole.

Mambo Mengine ya msingi kuzingatia

1. Lugha:   
Lugha ndio kiungo cha mawasiliano, kwahiyo ni muhimu kutambua lugha kuu ya mawasiliano ya eneo husika, na kujitahidi kuweza kuzungumza kwa ufasaha na pia ujiandae kujifunza lugha ndogo za mawasiliano ya kila siku. Mfano mzuri wengi hujidanganya na ‘Kiswanglish’ yaani kule kuzungumza kiswahili kisha ukachomekea na maneno machache ya kiingereza basi ndio ukajiona unaifahamu lugha. Jitahidi uiweze vema lugha husika kwani huko uendako hautopata muda wa kuchanganya kiswahili na lugha ya kigeni.  Hata hivyo ni jambo la kukumbuka ukiwa makini na kwa jitihada za uhakika, utaweza kujikuta unaifahamu vema lugha ngeni kwa haraka.

2.Utofauti wa tamaduni: 
Kuna tofauti nyingi za jinsi watu wanavyoishi katika nchi nyingine , mfano aina ya vyakula wanavyokula, mavazi,  jinsi wanavyoheshimiana, kusalimiana, kuabudu,  aina za nyumba, usafiri, n.k Uwe tayari kukabiliana na utofauti huo wa tamaduni na ujifunze kuheshimu tamaduni za wengine.

3. Gharama za maisha: 
Inapendeza zaidi ukifanya utafiti wa gharama za maisha za nchi husika unayotarajia kuishi ili kujua jinsi kipato chako kitakavyotumika na jinsi utakavyoweza kuweka akiba kwa ajili ya shughuli nyinginezo za ndoto zako. Nchi nyingi zilizoendelea zina gharama kubwa za maisha hivyo kujikuta unaishia kutumia sehemu kubwa ya mapato yako kwa kula na kujikimu tuu.

4. Ajira ni bidhaa:  
 Mtu,shirika au kampuni, hutangaza nafasi ya kazi ili kuweza kupata mtu atakayefanyika shughuli fulani kwao. Hivyo kuendana na ujuzi wako na uzoefu wako, unajikuta unatakiwa uwahakikishie au uwaridhishe hao waajiri kuwa kweli utaweza kufanya hayo wanayotaraji wewe kufanya. Hii ni kama kuuza bidhaa, ambapo ni lazima kumfanya mteja aone sababu ya kununua bidhaa yako. Andaa vema wasifu wako (CV/RESUME), andika kwa ufasaha barua ya maombi ya kazi ukijieleza vema kwa kulinganisha maelezo ya nafasi husika unayoomba, uzoefu wako  na ujuzi wako. Usikate tamaa pale maombi yanapokosa majibu, endelea kuaply sehemu nyingine.

5. Utayari wa kuishi katika nchi husika: 
Inapendeza pia ukapata taarifa za awali kuhusu nchi husika unayofikiria kufanya kazi. Tumia mitandao ya kijamii, websites na hata mawasiliano ya moja kwa moja ya watu waishio huko ili kujua hali ya hewa, tamaduni, gharama za maisha na mambo mengine unayoona yanaweza kuathiri maisha yako. Pia ukiwa na nafasi wewe mwenyewe funga safari uende kuitembelea nchi husika ukae walau mwezi mmoja au wiki kadhaa hivi, ili kujifunza zaidi kuhusu nchi husika na kujipima kama kweli upo tayari kuishi nchi husika.
N:B: Maelezo haya si ushauri binafsi kwako msomaji kuhusu kupata ajira. Lengo ni kutoa tuu mtazamo wa mwandishi wetu kuhusu soko la ajira nje ya Tanzania.